Friday, February 27, 2015

Tunaelimishaje watoto wetu na wa jirani zetu? NO. 5b




      “Mazingira magumu” neno mazingira pia lina maelezo mengine yakufanana nalo ambayo ni mandhari, hali, zunguka, zingira, zingia, na zinga. Hivyo “magumu” ni kivumishi cha kuoneshea ni kwa namna gani hayo mazingira yalivyo. Kama ukisema ni hali ngumu pia inaendana na dhana nzima ya mazingira magumu katika hoja yangu ya msingi.

    Mazingira magumu huwa yanatofautiana kati ya kaya moja na kaya nyingine, watoto wanaoishi katika mazingira magumu wana tofautiana pia katika hali wanazopitia katika maisha yao. Kupata wazazi au walezi wasiothamini elimu wala kuona umuhimu wa watoto kupata elimu, ni mazingira magumu ya awali ambayo kwa namna ya kipekee hayawezi kumpa mtoto hamasa ya kupenda kusoma.

   Katika makala zilizotangulia niligusia suala zima la upendo wa wazazi kwa mtoto, mama na baba na ndugu wa karibu wa familia wana nafasi kubwa katika kumjengea mtoto mazingira mepesi kuelekea mafanikio yake ya kielimu. Tukumbuke watoto wanazaliwa wakiwa na uwezo wa kiakili na ufahamu wa kiasi tayari kwa kuanza kujifunza mambo mengine kadiri ya mazingira atakayokutana nayo.

    Agizo kuu la awali la Mungu kwa Adamu na Eva ilikuwa ni la kuzaa na kuongezeka ili wapate kuijaza dunia, hivyo uwepo wetu hapa duniani wa mtu mke na mtu mume ni katika kutimiliza upendo huo mkuu toka kwa Mungu. “Kuzaa si kazi, kazi kulea mwana” ni msemo wa kawaida sana kuusikia linapokuja suala la mjadala kuhusu watoto na malezi yao. Tatizo kubwa lililopo ni kwenye tafsiri ya maneno yanayotumika katika suala zima la mawasiliano, ukichukulia kauli hiyo ya kazi kulea mwana kila mmoja anaweza kuwa na fikra tofauti lakini mimi naweza kukwambia kulea ililenga katika dhana ya kumwelimisha mtoto.

       Mungu ndiye chanzo cha maarifa yote, Mungu ni hekima ipitayo hekima zote katika kuona ukweli huo katika kitabu kitakatifu cha Biblia katika kitabu cha Mithali, “Watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa” ni kauli aliyotoa Mwenyezi Mungu ikionesha umuhimu wa maarifa ili watu wa Mungu wasiangamie. Katika hili ndipo wazo la Baba na Mama ni miungu wa dunia usije kulisahau na kulipuuzia. Kwani Baba na Mama ni wa kwanza katika kuhakikisha mtoto wao anapata maarifa stahiki, nadhani ndugu msomaji umeanza kupata picha sasa ya namna ya kutenda kadiri inavyopasa.

      Mazingira magumu yanaweza kufanana na haya yafuatayo, mtoto kutozungukwa na watu wenye mwamko wa kielimu, ikiwemo mtoto kuzaliwa katika ukoo usio na mwamko wa kielimu, mtoto kuzaliwa katika familia hohehahe yenye kipato duni kisichotosheleza hata kupata mlo wa siku moja. Mtoto kulelewa na mzazi mmoja iwe baba au mama, mtoto kulelewa na bibi na babu, mtoto kulelewa na ndugu na jamaa, mtoto kuzaliwa katika eneo lenye utamaduni usiojali elimu, mtoto kuzaliwa katika eneo lenye mtazamo hasi kuhusu masuala ya kielimu, mtoto kuzaliwa katika wakati ambao Taifa halina mwelekeo mzuri wa kielimu wala mipango ya kujikwamua katika kuwekeza kwenye elimu ya watoto. Hiyo ni mifano ya baadhi tu ya mazingira magumu ambayo yanachangia kwa kiasi kikubwa kurudisha nyuma maendeleo ya kielimu ya mtoto.

Kila aina ya mfano wa mazingira magumu unaweza kupata maelezo mengi tofauti kwa kuwa namna ya kukabiliana na mazingira hayo pia inatofautiana kati ya mtu mmoja na mwingine. Jambo la msingi kabisa ni mwamko wa kielimu wa jamii husika ambayo mtoto huyo atakuwa amezaliwa. Jamii hiyo inachukuliaje suala zima la elimu? Kwa namna ya kipekee katika hoja hii nitapenda kuelezea pia na uzoefu wangu katika maisha haya tunayoweza kuita ya mazingira magumu.

Kijana “Kung’alo” jina la kubuni, ni mzaliwa wa kaya duni kama zilivyo kaya nyingi za hapa Tanzania amepitia katika mazingira mengi magumu ya kimaisha. Lakini kwa upendo na msaada mkubwa wa Mungu ameweza kujifunza masuala mbalimbali ya kijamii.  Katika familia yao walizaliwa watoto takriban nane (8) katika jiji la Dar es salaam, jiji lililojaa kila aina ya pilika tangu enzi za utawala wa awamu ya kwanza baada ya kupata uhuru.

Wazazi wao hawakuwa waajiriwa, ni baba ndio alikuwa chanzo cha kipato cha familia kwa hivyo kulikuwa na changamoto mbalimbali katika maisha ya familia hiyo. Kung’alo akingali mdogo yeye na ndugu zake baba yao alianza kuingia katika ulevi wa kupindukia ambao kwa namna kubwa ulisababisha kuyumba kwa familia kwani kipato kidogo alichokuwa akipata baba huyo, pia kilifanyiwa matumizi mengine ya anasa za dunia.

Wakati wa kuanza kujiunga na shule ulipowadia kadiri ya umri wa Kung’alo ambaye ndie alikuwa wa kwanza kuzaliwa alienda kuanza darasa la kwanza. Wakati huo umri wa kuanza darasa la kwanza ilikuwa ni miaka 9 na 10, akawa na maendeleo mazuri darasani alipofika darasa la tatu na mdogo wake Kung’alo alianzishwa darasa la kwanza na yeye. Familia hiyo ilikuwa na utaratibu huo wa kuwapishanisha madarasa mawili watoto wao ikishabihiana na tofauti yao ya umri wa kuzaliwa.

Watoto wa kaya hiyo walikuwa na uwezo mkubwa wa kiakili kwani walikuwa na maendeleo mazuri katika masomo yao tangu ngazi ya awali. Maisha yao yakazidi kuwa magumu kwa vile sasa mahitaji yakawa mengi zaidi yakiongezeka na gharama za shule, kwani ili watoto waendelee vema na masomo kuna wakati walilazimika kwenda twisheni na kufanya mitihani mbalimbali ya majaribio. Kwa hakika pongezi kubwa inastahili kwenda kwa mama yao mzazi bwana Kung’alo na wadogo zake. Mama huyo alihakikisha watoto zake wanapata elimu, alikuwa na juhudi kubwa ya kufuatilia mwenendo wa watoto zake.

Mama huyo alikuwa na utaratibu wa kuwatambua walimu wa darasa kwa kila mtoto wake, hivyo kwa utaratibu huo aliweza kufahamiana na walimu wengi sana shuleni walipokuwa wanasoma watoto zake. Jambo la kipekee ni kwamba mama huyo aliamua watoto zake wote wasome katika shule hiyo hiyo, nadhani akiwa na lengo madhubuti la kuwafuatilia kwa ukaribu zaidi kuliko wangekuwa kila mmoja anasoma katika shule tofauti. Alishiriki kila kikao cha wazazi wa wanafunzi pale walipokuwa wanahitajika kufika shuleni kusikiliza mipango ya shule hiyo.

Wakati wote huo baba yao kina Kung’alo yeye alikuwa akiendelea na mabadiliko yake ya maisha ya anasa ilhali kipato chake pia hakikuwa cha kuridhisha. Kadiri hali ilivyozidi kuwa ngumu, ndipo mama yao kina Kung’alo akaanza kujishughulisha na biashara mbalimbali ndogondogo katika jitihada za kupunguza ugumu wa maisha na kupata pesa za kusaidia maendeleo ya watoto shuleni. Kung’alo na wadogo zake nao hawakuwa nyuma wakisaidiana na mama yao katika kutafuta ridhki kwa ajili ya mahitaji ya familia. Mungu akaendelea kuwajalia vijana hao, wakaendelea vema na masomo yao bila ya kukatishwa tamaa na mazingira waliyokuwa nayo.

Kung’alo alifanikiwa kufaulu vema katika mitihani yake ya darasa la saba na kuchaguliwa kwenda sekondari, kwa wakati huo jambo kama hilo lilikuwa ni la kipekee waliokuwa wanafaulu na kuchaguliwa walistahili kwelikweli kwa vile walikuwa na akili na vipaji sana. Na kwa hali ya ufinyu wa shule kwa wakati ule idadi ya waliochaguliwa ilikuwa ni ndogo sana, lakini haikuwa kwa kijana huyo Kung’alo.
Ikawa hivyo hivyo na kwa wadogo zake Kung’alo walifanikiwa kupata nafasi ya kuendelea na elimu ya sekondari, ikawa ni furaha kubwa kwa mama yao hasa juhudi kubwa aliyoifanya kuhakikisha watoto zake wanasoma. Baba yao alikuwa akijivunia vipaji vya watoto hao kwa kujinadi kuwa amefanikiwa kuwasomesha watoto zake, kinyume na hali ilivyokuwa kwani ni mama yao ndio alikuwa shujaa wa elimu yao. Hata walipokuwa wakilala bila ya kula mlo wa usiku lakini bado vijana hao walilazimika kuamka mapema na kuwahi namba shuleni.

Ni kama walitambua kwamba elimu ndio itakuwa mkombozi wa familia yao kwa siku zijazo, walikuwa na juhudi kubwa ya kusoma wakichagizwa na uwezo mkubwa wa kiakili waliozaliwa nao. Mazingira mbalimbali ya kukatisha tamaa walikumbana nayo ikiwemo ya kukosa chakula iwe asubuhi, mchana na usiku lakini linapokuja suala la shule walikuwa mstari wa mbele. Walikosa pesa ya kulipia twisheni, walikosa ada, upatikanaji wa ada ulikuwa ni wa kukatisha tamaa walipokuwa katika shule za sekondari lakini waliendelea kupenda elimu.

Kuzaliwa katika mazingira magumu sio kigezo pekee cha mtoto kushindwa kufanya vema katika masomo yake, lazima viwepo vichocheo vingine vya kufanya ugumu huo ukawa kikwazo. Katika maelezo yote ya makali hii ukiangalia unagundua kwamba huwezi kufanya jambo lolote pasipo kuwa na sehemu ya kusimamia. Hata wajenzi wa nyumba huwa wanaanza na msingi katika kusimamisha jengo lao, ndivyo ilivyo kwa mtoto anayezaliwa katika mazingira magumu ili aweze kuendelea vema ni budi apate sehemu ya kusimamia.

Kuwepo na mtu wa kumsimamia na kumwongoza, ni kweli wapo wanaozaliwa na kipaji cha kujipa motisha na hamasa wao wenyewe. Watu wa aina hiyo wanao uwezo wa kusaka msaada popote pale wanapoona panafaa, ila kwa kiasi kikubwa tunao watoto ambao hawana vipaji vya namna hiyo. Na hakuna wataalamu wa kuwezesha utambuzi wa jambo hilo, walimu wetu hawaandaliwi kufanya jambo hilo kwa watoto wala wazazi wao.

Lakini ukweli wa jambo hili ni kwamba, inawezekana kabisa kumtambua mtoto amezaliwa kuwa nani katika maisha yake yajayo, zipo elimu nyingi za kuwezesha utambuzi wa jambo hilo, kuna elimu za saikolojia, filosofia, sosholojia, elimu ya unajimu na malezi mbalimbali. Wazazi ndio wangekuwa wa kwanza sasa kupewa maarifa hayo ili wajue namna ipasayo kulea watoto wao, elimu hiyo wazazi wanaweza kuipata kupitia viongozi wao wa dini, kupitia waelimishaji rika, na wafanyao kazi za kutoa ushauri wa malezi.




Nb: Mada hii itakuwa na mwendelezo wake kwa kuendelea kujadili suala la elimu kwa mapana yake, ili wazazi na wadau wa elimu kupata nuru ya kufanya maamuzi sahihi.

By Mkoba Andrian.

0 comments:

Post a Comment