Friday, February 20, 2015

Tunaelimishaje watoto wetu na wa jirani zetu? NO. 5





“Kama elimu ni ghali, jaribu ujinga” sio msemo mgeni huu masikioni mwako, hilo naamini ni jambo lililo wazi kabisa kwetu sote ya kwamba elimu ni ghali hasa katika maisha ya sasa. Elimu imekuwa ghali sana kutokana na mabadiliko mbalimbali ya kimaisha duniani kote na hapa Tanzania pia. Kipindi cha ukoloni na miaka ya mwanzo ya uhuru elimu ilitolewa bure kwa wananchi kwa kuwa idadi kubwa ya watu ilikuwa haina elimu ya kimagharibi.

Na pia kulikuwa na idadi ndogo ya watu hivyo serikali iliweza kumudu kugharamia maisha ya watu wake katika upatikanaji wa elimu na masuala mengine ya kijamii. Kumbuka katika makala ya awali nilizungumzia kuhusu aina kuu tatu za elimu, linapokuja suala la elimu rasmi basi moja kwa moja tunazungumzia elimu yenye asili ya kimagharibi. Hivyo kwa upatikanaji wa aina hiyo ya elimu tunaingia rasmi katika mfumo wa maisha ya kimagharibi, kwa hiyo hakuna namna ya kukwepa moja kwa moja gharama ya elimu kwa kuwa upatikanaji wa elimu hiyo ni wa gharama.

Kwa kuzingatia hilo la gharama ya upatikanaji wa elimu rasmi, ndipo tuendelee kujadiliana hoja yetu ya msingi kuhusu namna ya kuelimisha watoto wetu na wa jirani zetu. Katika hili nianze kusema wazi kabisa watoto wengi huwa wanazaliwa wakiwa safi kabisa katika afya zao za mwili, roho na akili. Ingawa pia wapo kwa idadi ndogo wale wanaozaliwa wakiwa na hitilafu. Kila mtoto anapozaliwa huwa amezaliwa kutimiza lengo maalumu nikiwa na maana ya mtoto wako ndugu msomaji na mtoto wa jirani yako pia. Hivyo kwa pamoja watoto hao ndio wanaweza kuendeleza gurudumu la maendeleo yao na ya jamii kwa ujumla wake.

Akili ya mtoto anapozaliwa haina uhusiano wowote na uwezo wa kiuchumi wa wazazi waliomzaa. Ila kuna uwezekano mkubwa wa mtoto huyo kuwa na vinasaba vya akili inayofanana na hao wazazi wake waliomzaa. Kumbuka ule msemo maarufu wa “Mtoto wa nyoka ni nyoka” nao unaweza kuleta maana katika maelezo yangu hapa kuhusu akili ya mtoto kurandana na ile ya wazazi wake. Kama mwanazuoni wa kijapani Okumura (2010) alivyoelezea katika ripoti yake ya utafiti juu ya ushawishi wa wazazi katika tabia za watoto wao. 

Ni wazi sasa unaweza kujiuliza maswali kadhaa ikiwa suala zima la elimu linakuwa hivyo je watu walio maskini wa kipato na watoto wanaoishi katika mazingira magumu wanawezaje sasa kupata tunu ya elimu kama ilivyo kwa watoto wanaozaliwa katika mazingira mazuri ya kipato? Pamoja na maswali mengine yafuatayo;

·         Jukumu la elimu ni la nani?
·         Watoto wanaoishi katika mazingira magumu ni jukumu la nani kuwapatia elimu?
·         Jamii inawapokeaje watoto wanaoishi katika mazingira magumu?
·         Mazingira magumu ni yepi kwa watoto?
·         Nani anasababisha mazingira magumu kwa watoto?
·         Nini wajibu wa serikali kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu?

Hayo ni miongoni mwa maswali ambayo kama mwana jamii unaweza kujiuliza na kuona ni kwa namna gani unaweza kuwa mwanaharakati wa elimu ya watoto wako na wa jirani yako. Ni kweli tunao wajibu wa kubadilisha namna yetu ya kufikiri kuhusu elimu na maendeleo ya jamii yetu.
Neno mazingira magumu linaweza kukosa maelezo ya moja kwa moja kumuelewesha mtu mpaka akaelewa, ila kwa faida ya hoja yangu ya msingi itoshe kusema ni hali ya umaskini wa kipato uliokithiri unaomkabili mtoto na familia inayomlea. Kwa hapa nchini kwetu Tanzania zipo kaya ambazo zinaishi kwa pato la chini ya dola moja ya Kimarekani. Ni kawaida katika Nyanja ya kiuchumi kufanya ulinganifu wa hivyo kuhusiana na kipato cha kaya moja na nyingine.

Watoto wanaoishi katika mazingira magumu wana changamoto kubwa katika suala la upatikanaji wa elimu, wanakosa mambo mengi ya msingi ikiwemo motisha ya wao kupenda maisha ya kujifunza kama ilivyo kwa watoto wengine wa rika lao. Wanakosa vifaa muhimu vya kuwawezesha kumudu changamoto za kielimu mfano; sare za shule, viatu, madaftari, kalamu, vile vile kwa wanaokaa mbali na shule suala la usafiri na upatikanaji wa chakula.

Mwanafalsafa wa kigiriki anayeheshimika sana duniani katika masuala ya kielimu alipata kunena mtu aliye na njaa hawezi kumudu kufanya tafakari nzuri. Kwahiyo ni wazi inahitaji mtu aweze kuwa na amani ya nafsi na mwili wake kwa ujumla ili aweze kumudu suala zima la kushiriki katika kujifunza. Unapozungumza kuhusu mtoto anayeishi katika mazingira magumu huwa anapitia maangaiko makubwa sana ya kimaisha ambayo ni ngumu sana kumpa motisha ya kupenda kufuatilia masomo.

Mazingira magumu ni magumu hasa, kwani mtoto anapotoka shuleni baada ya kazi kubwa ya kujifunza aliyoifanya akiwa shuleni, arudipo nyumbani angependa akute mazingira mazuri yaliyo rafiki. Ikiwemo wazazi ama walezi wenye furaha na amani, akute chakula cha kumuwezesha kurudisha nguvu yake aliyoipoteza shuleni. Lakini mazingira hayo ni nadra kwa watoto hao wanaoishi katika mazingira magumu hilo kwa kiasi kikubwa linachangia watoto hao kuchukua uamuzi wa kuacha shule ili waweze kupata muda wa kujitafutia pesa za kujikimu ikiwemo na kulea familia zao pia.

Katika jamii zetu wapo watoto wadogo wanao wajibika kutunza familia zao, bila kujali huo umri wao mdogo. Kaya maskini kwa hakika zina msukumo mbaya kwa maisha ya watoto wao. Wapo watoto wanaoingia katika ajira zisizo rasmi ikiwemo wizi na biashara ya ukahaba ili waweze kupata pesa za kusaidia familia zao.

Ni jambo linalohitaji mkakati mzuri wa kimaendeleo kwa jamii yetu kuona umuhimu na namna nzuri ya kuweza kusaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu ili kuepushia taifa letu janga kubwa linaloweza kutokea kwa kuwa na kundi kubwa la vijana lisilo na elimu stahiki. Ingawa si nia ya hoja yangu lakini si vibaya nikisema tukio lililotokea la vijana wanaojiita “Panya Road” ni ishara ya jamii iliyokithiri katika hali duni ya kimaisha. Kwa kuwa kundi kubwa la vijana waliostahili kuwa shuleni na wengine vyuoni ndio hao wanaoshiriki katika vitendo vya uhalifu.

Bila juhudi ya makusudi kukabiliana na suala hilo la kuwapatia watoto na vijana wetu elimu, basi tutarajie mambo kama hayo yakitendeka mara kwa mara. Hivyo kwa namna moja ama nyingine hata waliopata nafasi ya kusoma hawatakuwa tena na amani ya maisha yao kwa kuwa wale wasiosoma watahitaji kugawana nao pato lao kwa kutumia nguvu zao kwa kuwakaba na hata kuwaua.


Nb: Mada hii itakuwa na mwendelezo wake kwa kuendelea kujadili suala la elimu kwa mapana yake, ili wazazi na wadau wa elimu kupata nuru ya kufanya maamuzi sahi

0 comments:

Post a Comment