Saturday, January 24, 2015

Tunaelimishaje watoto wetu na wa jirani zetu? NO. 3



Tunaelimishaje watoto wetu na wa jirani zetu?   NO. 3
“Mtoto wa nyoka ni nyoka” Nitashangaa ukiniambia hujawahi kuusikia msemo huo katika pitapita zako ama wakati ukiwa mwanafunzi na wewe. Lakini nikikuuliza maana halisi ya msemo huo unaweza kunipa majibu mengi tofauti kwa kuwa hiyo imebeba lugha ya picha ndani yake. Nikisema lugha ya picha naomba nieleweke vema kwamba ni kauli ambayo imeficha ujumbe wake halisi, na kumuachia msomaji ama msikilizaji kuupatia maana yeye mwenyewe.

Lugha ni nini? Kuna maelezo mengi tofauti yanayoweza kuleta maana ya neno lugha, lakini itoshe kusema lugha ni chombo cha mawasiliano ambapo utokea kwa bahati nasibu ikiwa na lengo la kuwezesha mawasiliano kati ya mtu mmoja na mwingine ama kundi la watu. Watoto nao hawako nyuma katika matumizi ya lugha kama ilivyo katika makundi mengine ya watu.

Watoto huwa wanazaliwa wakiwa na uwezo maalum wa kutambua lugha ya mawasiliano katika jamii yao, kama mtaalam aliyebobea katika masuala ya lugha za dunia alivyopata kusema katika machapisho yake mbalimbali aliyofanya kuhusu lugha. Chomsky (1980)

Kila mtoto anazaliwa akiwa na uwezo wa kuelewa lugha, ni kama tulivyokwisha soma katika makala za awali namna elimu inavyoweza kupatikana. Unaweza kutafakari jambo hili ni mara ngapi umeshasikia watoto wadogo wajifunzao kuzungumza wakiita maji kwa jina la “MMA?” unaweza kuwa na majibu kwa swali hilo. Na endapo utakosa jibu basi nichukue nafasi hii kukusihi uwe unatumia muda wako kukaa jirani na watoto wajifunzao kuzungumza uweze kushuhudia namna wanavyofanana katika matamshi yao ya awali.

Lugha ni chombo cha mawasiliano wote tunaweza kukubaliana hivyo, watoto nao wanatumia lugha katika kuwasilisha mahitaji yao kwa wazazi na wale wanaowalea. Watoto wanajifunza lugha kwa njia mbalimbali katika mazingira yao. Ni changamoto kubwa sana kwa wazazi katika kuhakikisha watoto wanapata ufahamu wa lugha zinazotumika katika jamii yao.

Watoto wana nafasi kubwa kuliko kundi lingine lolote katika kujifunza lugha kwa vigezo mbalimbali, cha muhimu ni watoto kupewa nafasi na wazazi wao. Watoto wanatakiwa kupewa nafasi ya kucheza na wenzao kwa muda mrefu zaidi ili waweze kupata wakujifunza nao lugha yao. Maneno mapya wanaweza kuyapata wakiwa katika kundi la watoto wenzao ambapo maneno hayo wataenda kuwauliza wazazi wawapatie ufafanuzi.

Ili mtoto aweze kujifunza vema masuala yanayohusu jamii yake ni budi lugha ya jamii hiyo ifahamike kwa mtoto huyo, kuhusu namna gani mtoto anaweza kujifunza lugha ya jamii yake. Ufafanuzi nimeutoa hapo juu, hivyo ni wajibu wa wazazi na walezi kuwapa nafasi watoto ili kuweza kujifunza lugha kupitia kundi la watoto wenzao.

Jamii yetu na taifa linakumbwa na changamoto kubwa kwa sasa kuhusu uamuzi wa lugha ya kutumika katika kuelimisha watoto. Nawe unaweza kuwa kati ya wadau wa elimu ukiacha sifa yako ya uzazi ama ulezi, unaweza kushirikiana na jamii katika kushauriana lugha ifaayo katika kuelimishia watoto. Lengo likiwa ni kuwezesha watoto hao kupata maarifa na taarifa kusudiwa.

Lugha ambayo ndiyo inatumika katika mawasiliano ya jamii husika ndio ingekuwa chaguo la kwanza katika kutumika kuelimisha watoto. Si vibaya kujifunza na lugha nyingine za kigeni katika kumuwezesha mtoto kupata ufahamu wa lugha nyingine pia.

Lakini lengo la elimu ambalo ni kuhaulisha maarifa na taarifa toka kizazi kimoja kwenda kizazi kingine ili litimie yumkini ikitumika lugha inayoeleweka kwa wote jambo hilo likafanikiwa. Tuonee fahari lugha ambayo watoto wetu wanaipenda na kuitumia kwa uhuru wakiwa na wenzao katika michezo yao inayowajenga kiakili na kimwili.

Tukumbuke lugha ni chombo cha mawasiliano, taarifa na maarifa yanaweza kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mtu mwingine kwa kutumia lugha. Lugha yenyewe si sehemu ya taarifa au maarifa hayo, nikiwa na maana mtu anaweza kuwa na uwezo wa kuifahamu lugha husika pasipo kuwa na maarifa wala taarifa sahihi kuhusu yaliyo muhimu kwa maendeleo yake.

Lugha isiwe kikwazo kwa kufanikisha suala la upatikanaji wa elimu bora kwa watoto wetu ambao ndio wataalamu tunaotarajia waweze kuleta mabadiliko katika jamii zetu. Elimu ni nguvu kubwa kwa yeye aliyefanikiwa kuipata. Tuwape watoto nguvu hiyo kwa kuwapa taarifa na maarifa sahihi kwa kutumia lugha sahihi inayofanikisha upatikanaji wa elimu.

Tupo kwa ajili ya watoto, na ifahamike wazi bila ya watoto hakuna jamii wala taifa mahali popote. Tutimize wajibu wetu wa kufanikisha maendeleo ya watoto.

Nb: Mada hii itakuwa na mwendelezo wake kwa kuendelea kujadili suala la elimu kwa mapana yake, ili wazazi na wadau wa elimu kupata nuru ya kufanya maamuzi sahihi.

 WRITTEN BY: ANDRIAN MUKOBA.








0 comments:

Post a Comment