Tuesday, December 30, 2014

Tunaelimishaje watoto wetu na wa jirani zetu ?


Tunaelimishaje watoto wetu na wa jirani zetu?

‘Elimu ni ufunguo wa maisha’ ‘ Elimu ni bahari’ ‘Elimu ni mkombozi’ ‘ Kama elimu ni ghali jaribu ujinga’ hizo ni semi ambazo tunakutana nazo mara kwa mara katika upashanaji habari na utafutaji habari kwenye maisha yetu ya kila siku.

Elimu ni kitendo kinachofayika kuhamisha taarifa, maarifa na ujuzi toka kizazi kimoja kwenda kizazi kingine. Mara nyingi ni kizazi kilichotangulia kwenda kizazi kinachofuatia lakini pia inawezekana kuwa kinyume chake. Elimu inawezekana kwa mwongozo wa mtu mmoja kumuongoza mwingine ama mtu kujiongoza mwenyewe katika kupata elimu husika.

 Elimu utolewa kwa namna kuu tatu ambazo ni namna rasmi, namna rasmi kiasi na namna isiyo rasmi kabisa. Naposema rasmi namaanisha namna ya utoaji wa elimu kwa utaratibu maalum uliopangwa na mamlaka za elimu katika nchi. Utaratibu unaweza kuwa umri, mazingira ya kujifunzia, kipindi cha mafunzo n.k  mfano wa mamlaka za elimu ni Wizara ya elimu yenye jukumu hilo hapa Tanzania. Baada ya kupata mafunzo yaliyokusudiwa mhitimu anapatiwa cheti cha kuthibitisha elimu aliyopata kwa utaratibu uliopangwa.

Elimu rasmi kiasi inatofautiana na nyingine kwa namna ambayo nayo utolewa kwa wanaojifunza, utaratibu wa elimu isiyo rasmi unatofautiana na utaratibu wa elimu iliyo rasmi kwa mambo kadhaa ikiwemo umri, mazingira ya kujifunzia, utolewaji wa vyeti kwa wahitimu na muda wa kujifunza mpaka kuhitimu mafunzo yaliyokusudiwa.

Elimu isiyo rasmi kabisa, ni ile mtu anaipata kupitia vyanzo mbalimbali katika mazingira tofauti tofauti na hakuna utaratibu maalum wa kujifunza. Hakuna utaratibu wa kupatiwa cheti kwa namna hii ya kujifunza kwa vile hakuna mtu anayewajibika kwa mwingine katika namna ya elimu ipatikanayo. Mfano wa elimu hii ni pale mama anapomfundisha mwanae kupika na kufanya kazi za usafi nyumbani, baba anapomfundisha kijana wake kazi ya uvuvi ama kusuka vikapu n.k

Ambacho tunapaswa kukifahamu ni kwamba, kila mtu anapitia katika namna zote za upatikanaji wa elimu kwa namna mbalimbali kupitia familia zetu, dini zetu, rika katika jamii zetu na kupitia jamii nzima ikiwemo mamlaka ya nchi. Pia kwa kupitia vyombo mbalimbali vya habari huwa tunajifunza masuala mbalimbali katika jamii zetu.

Tukirejea katika hoja ya msingi ambayo nimeifanya kama kichwa cha makala yangu, tunaweza sasa kujiuliza maswali mbalimbali kuhusu elimu, baadhi ya maswali hayo ni kama ifuatavyo;

·         Lengo la elimu ni nini?

·         Nani anawajibika kwa upatikanaji wa elimu?

·         Elimu gani ifaayo kutolewa kwa kila kundi katika jamii?

·         Mwenye elimu ana wajibu gani kwake na kwa jamii yake?

·         Jamii ina wajibu gani kwa mtoa elimu?

·         Mtoa elimu anastahili kuwa na sifa gani?

·         Njia gani ifaayo kutoa elimu?

·         Lugha gani ifaayo kutumika katika utoaji wa elimu?

Naamini unaweza kuona hapo maswali ni mengi mno tunayoweza kujiuliza, ni changamoto kubwa iko mbele yetu kuweza kupata majibu ya maswali haya na mengineyo kuhusu elimu.

Kwa kufahamu maana ya elimu na namna ya upatikanaji wa elimu tunaweza sasa kuona ya kwamba elimu ni sehemu ya maisha mwanadamu (mtu). Kwa maana ya kwamba mtu ni mwanaelimu, kila mtu anazaliwa kwa lengo la kuwa mwanaelimu kuanzia katika ngazi ya familia na hatimaye jamii kwa ujumla wake.

Ni vema sasa kuanza kuweka uzito katika jambo la elimu kwa kuwa lengo kuu la uwepo wetu hapa duniani ni kuwa na elimu ya kutosha (maarifa). Na kwamba sote ni ndugu kwa maana ya uumbwaji wetu. Tunao wajibu kwa ndugu wote katika ulimwengu wa elimu, kuhakikisha watoto wetu na watoto wa jirani zetu wanapata elimu stahiki kwa manufaa ya jamii zetu.

 

Nb: Mada hii itakuwa na mwendelezo wake kwa kuendelea kujadili suala la elimu kwa mapana yake, ili wazazi na wadau wa elimu kupata nuru ya kufanya maamuzi sahihi.
         
Written by : Mkoba  Adrian.

0 comments:

Post a Comment