Friday, February 6, 2015

JE MZAZI UNAYAJUA MAJUKUMU YAKO KWENYE MAENDELEO YA ELIMU ?



JE MZAZI UNAYAJUA MAJUKUMU YAKO KWENYE MAENDELEO YA ELIMU ?

Na Makirita Amani

Miaka ya hivi karibuni kumekuwa na anguko kubwa sana kwenye maendeleo ya elimu. Wanafunzi wengi sana wamekuwa wakifeli katika mitihani yao hasa ya kidato cha nne. Katika kufeli huku lawama nyingi sana zimetolewa kwa watu wanaohusika na kuporomoka huku kwa elimu.
Tumeona kila mtu akilaumu serikali kwa kutoweka kipaumbele kwenye maendeleo ya elimu. Serikali imelaumiwa kwa kujenga shule nyingi ambazo hazina walimu, vitabu au maabara. Na pia serikali imelaumiwa kwa kutojali maslahi ya walimu na hivyo walimu kufanya kazi kwenye mazingira magumu na hivyo kuchangia kushuka kwa elimu.
Tumeona pia walimu wakilaumiwa sana kwenye kushuka huku kwa elimu. Walimu wanalaumiwa kwa kutozingatia majukumu yao na hivyo wanafunzi kukosa masomo. Na pia walimu wanalaumiwa kwa kuwa na mgomo baridi ambao unapelekea wanafunzi kukosa usimamizi mzuri shuleni na hivyo kupunguza ufaulu.
Hayo ndio makundi mawili ambayo yamelaumiwa sana kwenye kushuka kwa elimu yetu. Je hawa tu ndio wanaostahili lawama? Je upi ni mchango wa wazazi katika kukua na kuporomoka kwa elimu yetu? Ukweli ni kwamba wazazi wana nafasi kubwa sana katika kukua au kuporomoka kwa elimu. Kwa wanafunzi 
wanaosoma shule za kutwa, wanatumia muda mwingi nyumbani kuliko wanaotumia shuleni. Hii ina maana kwamba kama wazazi wangekuwa makini na maendeleo ya watoto wao shuleni wangekuwa watu wa kwanza kufuatilia kama watoto hawafanyi vizuri. Lakini hiki sio kinachotokea. Wazazi wamesahau kabisa majukumu yao na kuona walimu ndio wenye majukumu yote kuhusiana na elimu.
Ugumu wa maisha umewafanya wazazi kufanya kazi kwa muda mrefu na hivyo kukosa muda wa kufuatilia maendeleo ya watoto wao shuleni. Wazazi wanaamini kwamba kwa kulipa ada shuleni ndio wamekamilisha wajibu wao kwenye elimu. Hii sio sahihi kabisa.

Yafuatayo ni majukumu ya kila mzazi katika maendeleo ya elimu ya mtoto 

1.       Mzazi anatakiwa kujua vipaji vya mtoto wake. Mzazi ndio anakuwa karibu sana na mtoto hata kabla hajaenda shuleni. Kwa kuwa nae karibu anaweza kuona ni vitu gani mtoto anapendelea na hivyo kufanya. Kwa kujua vipaji vya mtoto kutamfanya mzazi aweze kuashauriana na walimu jinsi ya kuweza kuendeleza vipaji vya mtoto wake.

2.       Mzazi anatakiwa kujua maendeleo ya kila siku ya mtoto wake shuleni. Mzazi usisubiri ripoti ya nusu mwaka au ya mwaka kujua mtoto wako amekuwa wa ngapi darasani. Unatakiwa kufuatilia maendeleo ya mtoto wako kila siku. Jua ni kazi gani amepewa za kufanya nyumbani na hakikisha amezifanya kwa usahihi. Pia mzazi anatakiwa kujua maendeleo ya mtoto wake kinidhamu, maana bila nidhamu mtoto hawezi kufaulu vizuri.

3.       Mzazi anatakiwa kujua changamoto ambazo mtoto anazipitia shuleni. Inawezekana mtoto anaonewa na wanafunzi wenzake ila anaogopa kumwambia mwalimu kwa sababu ataonewa zaidi. Wewe kama mzazi ukiwa na urafiki na mtoto wako itakuwa rahisi kuona pale ambapo anapitia changamoto mbalimbali. Kwa kujua hivyo unaweza kuangalia njia nzuri inayoweza kumsaidia mtoto wako ili aweze kuwa na mazingira mazuri shuleni.

4.       Mazazi anatakiwa kumjengea mtoto wake mapenzi mazuri na elimu ili mtoto awe na mtizamo mzuri kuhusu elimu. Mzazi anatakiwa amweleze mtoto kwa nini ni muhimu kwake yeye kusoma na kufaulu vizuri. Pia ampe moyo pale ambapo anashindwa na kumhamasisha kuweka juhudi zaidi kwenye masomo yake.
5.       Mzazi anatakiwa kumfundisha mtoto mambo ambayo hapati nafasi ya kufundishwa shuleni. Sio mambo yote muhimu kwenye maisha mtoto anafundishwa shuleni, kama mzazi atapata nafasi ya kukaa na mtoto wake anaweza kumfundisha mambo ya ziada ambayo yatamsaidia shuleni na hata kwenye maisha.

Mzazi una jukumu la kwanza kabisa katika maendeleo ya mtoto wako kielimu. Acha kukwepa majukumu yako kwa kufikiri kwamba kulipa ada kubwa kunatosha wewe kumsaidia mtoto wako kwenye elimu. Maendeleo ya elimu yanahitaji ushirikiano mkubwa sana kati ya mwanafunzi, mzazi, mwalimu na serikali. Kila mmoja acheze nafasi yake ili tuweze kuendeleza elimu yetu

1 comment:

  1. Tatizo ni kwamba wazazi wengi nchini hasa wanaoishi katika mazingira magumu hawajui majukumu yako. Na inamfanya mzazi ajue kulipa ada na kununua mahitaji mengine ya shule kwa mtoto ndio wajibu wake na akifanya hivyo basi hana majukumu mengine katika maendeleo ya mtoto wake. Kwahiyo ni bora zaidi kama serikali na wadau mbalimbali wa elimu watawasaidia wazazi kujua majukumu yako katika maendeleo ya elimu

    ReplyDelete